WAKULIMA Mkoani Tabora wahimizwa kulima kwa kuzingatia kanuni za kilimo bora na kuzingatia Kalenda ya kilimo ili waweze kupata mazao bora ambayo yatawawezesha kuwaletea maendeleo yao na Taifa kwa ujumla.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Dkt. Philemon Sengati wakati wa uzinduzi wa msimu wa kilimo uliyofanyika wilayani Igunga.
Alisema kalenda ya kilimo inawataka wakulima wawe wameshalima na kupanda mazao mbalimbali ambayo hayahimili ukame kabla ya tarehe 15 ya Desemba ili mavuno yaweze kuwa mazuri.
Mkuu huyo wa Mkoa alisisitiza kwa wakulima wote ambao hawajandaa mashamba yao kufanya hivyo mapema ili waweze kulima kwa wakati na kupanda mbegu bora ili kupata mazao bora.
Dkt. Sengati aliwataka Maofisa Ugani kutumia muda huu kupeleka elimu hiyo na kuzingatia kalenda ya kilimo na kanuni za kilimo kwa wakulima ili uzalishaji wa mazao mbalimbali mkoani humo uweze kuongezeka na kuwapaisha kiuchumi wananchi.
“ Maofisa Kilimo na Maafisa ugani watoke maofisini na kwenda kwa wakulima kuwafundisha jinsi ya kulima kilimo kilicho bora na matumizi ya mbegu bora na mbolea kwa ajili ya kuinua uzalishaji wa mazao yao” aliagiza
Alisema uzalishaji wa mazao bora na kwa wingi utawawezesha wakulima nao kushiriki kikamilifu katika kushiriki katika uchumi wa kati na wa viwanda wakati Tanzania inaelekea kwenye uchumi wa juu.
“Bila kulima hatuwezi kuwa maendeleo ya kweli na tunapokuwa na maendeleo ya kweli ina maana tunaendelea kuwa na amani …maeneo mengi yenye umaskini yanagubikwa sana na migogoro.. wakulima limeni kwa wingi ili muwe na uchumi mpana” alisisitiza.
Dkt. Sengati aliwataka kuunga mkono falsafa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli ya hapa kazi kwa kupanua kilimo kupitia matumizi ya wanyama kazi na matrekta ili uzalishaji uongezeke.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa