WASOMI NCHINI KUANDIKA HISTORIA UPYA HISTORIA YA UKOMBOZI WA TANZANIA
WASOMI wa Kitanzania kutoka Vyuo Vikuu wametakiwa kuandika historia ya Watanzania mbalimbali waliotoa mchango mkubwa katika kupinga ukoloni nchini ili vijana waweze kupata picha halisi ya harakati za mapambani dhidi ya wakoloni.
Kauli hiyo imetolewa leo wilayani Urambo na Waziri wa Habari, Utamaduni , Sanaa na Michezo Dkt. Harrison Mwakyembe wakati wa ziara ya kikazi ya kutembelea maeneo ya urithi wa historia ya ukombozi wa Bara la Afrika.
Alisema waandishi wengi waliondika historia ya Tanzania ikiwemo mapambano dhidi ya ukoloni walitoka nje ya nchi na kuandika kwa matakwa yao na hivyo kuacha baadhi ya mashujaa wengi waliopinga kutawaliwa na wakoloni bila kuandikwa.
Dkt. Mwakyembe alisema katika mikoa mbalimbali imebainika kuwepo kwa watu walitoa upinzani mkali kwa Wajerumani na Waingereza lakini hakuna sehemu wanapotajwa katika vitabu wa historia za nchi ya Tanzania.
“Kuna mama Liti kutoka Singida alipambana na Wajerumani kwa kutumia nyuki lakini hakuna vitabu wa historia vinavyomzungumzia…kuna mama mmoja Manyoni ambaye yupo hai hadi leo alimuokoa Mwalimu Nyerere asikamatwe na Waingereza baada ya kumvalisha baibui na kisha kuungana naye lakini hakuna alipoandikwa” alisema.
“Mtemi Isike ni miongoni wa viongozi waliotoa upinzani mkubwa kwa Wajerumani na baadae akajipiga risasi kwa kukataa kukamatwa na Wajerumani , lakini hakuna vitabu vya historia vinapoeleza…tuna utajiri wa historia kubwa lakini iliyosndikwa ni sehemu kidogo sana” aliongeza.
Alisema hatua hiyo imesababisha vijana wengi kutokuwa na historia kubwa ya wapigania uhuru hapa nchini.
Dkt.Mwakyembe alisema wakati umefika wa Wasomi na wataalamu waliopo katika Vyuo vikuu mbalimbali hapa nchini kukaa chini na kufanya utafiti na kuandika historia ya urithi wa ukombozi hapa nchini kwa ajili ya kizazi cha sasa na kijacho.
Mmoja wa Wazee wa Urambo John Samwel alisema Serikali imefanya vizuri kuanza kuyatambua maeneo ya urithi wa kihistoria ya ukumbozi kwa ajili ya kuandika historia ya pana ya mapambano dhidi ya ukoloni nchini Tanzania.
Alisema hatua hiyo itasaidia kuondoa upotoshaji uliofanywa na waandishi kutoka mataifa ya nje ya bara la Afrika ikiwemo kudai uvumbuzi wa Ziwa Victoria , Mlima Kilimanjaro kugunduliwa na wazungu wakati walikuwepo Watanzania wenyeji wa maeneo hayo.
Samwel alisema ni vema historia iandike ukweli ili kuepuka kuwapotosha vijana na vizazi vijavyo.
Mwisho
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa