TABORA – Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya uongozi wa Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuonesha dhamira yake ya kuinua elimu ya juu na sekta ya kilimo nchini baada ya kukabidhi matrekta mawili kwa Chuo Kikuu Kishiriki cha Askofu Mihayo cha Tabora (AMUCTA). Hafla hiyo ya makabidhiano imeongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mhe. Paulo Chacha, katika viwanja vya chuo hicho, ikihudhuriwa na wanafunzi, viongozi wa chuo, pamoja na viongozi kutoka ngazi ya mkoa na wilaya.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mkuu wa Chuo Kikuu Kishiriki cha AMUCTA, Rev. Prof. Juvenalis Asantemungu, ametoa shukrani za dhati kwa serikali, hasa kwa Waziri wa Kilimo, Mhe. Hussein Bashe, kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora kufanikisha upatikanaji wa matrekta hayo. Profesa Asantemungu ameeleza kuwa msaada huo umetokana na ombi rasmi walilowasilisha kwa Waziri Bashe alipohudhuria mahafali ya kumi ya chuo hicho kama mgeni rasmi mnamo Novemba 23, 2024.
Naye Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, Dkt. John Mboya, katika salamu zake za awali, alieleza kuwa changamoto ya msingi katika elimu ya juu kwa sasa ni kutokuwepo kwa mafunzo yanayokidhi mahitaji halisi ya soko la ajira. Alisema kuwa kupitia kitivo hicho kipya, AMUCTA itakuwa na mchango mkubwa katika kuandaa wahitimu watakaoweza kujiajiri kupitia ujuzi kwa vitendo, hivyo kupunguza tatizo la ajira miongoni mwa vijana.
Mkuu wa Mkoa, Mhe. Paul Chacha, alitumia fursa hiyo kuipongeza AMUCTA kwa hatua yake ya kimkakati ya kupanua maeneo ya mafunzo. Alisema hatua hiyo ni kielelezo cha weledi na uongozi thabiti wa chuo hicho. Akimwakilisha Waziri wa Kilimo, Mhe. Bashe, Mkuu wa Mkoa alisoma ujumbe maalum kutoka kwa Waziri huyo, ukisisitiza kuwa msaada huo ni mwanzo wa ushirikiano mpana kati ya wizara na taasisi hiyo ya elimu. Aliwahakikishia viongozi wa chuo kuwa serikali iko tayari kushirikiana nao katika jitihada zote za kuendeleza elimu ya kilimo, na akawahimiza kuto kusita kuwasilisha mahitaji yao kwa serikali.
Kwa niaba ya jumuiya ya AMUCTA. Makamu Mkuu wa Chuo hicho,Rev.Prof. Emmanuel Wabanhu amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Mhe. Bashe kwa msaada huo mkubwa kwani utakwenda kuwanufaisha wanafunzi wa Imani zote kwani chuo hicho kinapokea watanzania wote bila kujali dini wala itikadi ya mtu.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa