MKUU wa Mkoa wa Tabora Balozi Dkt. Batilda Buriani amewataka Maafisa Maendeleo ya Jamii kutoa elimu ya Ujasiriamali kwa Walengwa wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii(TASAF) chini ya Mpango wa kunusuru kaya Maskini ili waweze kutumia fedha wanazopata kujiletea maendeleo.
Balozi Dkt. Batilda alitoa kauli hiyo leo wakati wa ziara yake ya kukagua shughuli zinazotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii(TASAF) chini ya Mpango wa kunusuru kaya Maskini katika Manispaa ya Tabora.
Alisema Walengwa wa Mpango wa kunusuru kaya Maskini wanatakiwa wapate elimu ya mbinu bora za ufugaji wa kuku ikiwemo namna ya kuwapa chanjo kwa ajili ya kuwakinga na magonjwa yanayowakabili na kuwafundisha juu ya ufugaji wa nyuki kupitia mizinga ya kisasa.
Balozi Dkt. Batilda alisema maeneo mengine ambayo wanapaswa kupewa elimu ni kuhusu uendeshaji wa biashara na uundaji wa vikundi kwa ajili ya uzalishaji mali.
Alisema hatua itawasaidia kufanyakazi kwa juhudi na kujiletea maendeleo hali itakayowafanya kuwachana fedha za TASAF na kutoa fursa kwa wahitaji wengine kupata fedha hizo.
“Mama yetu Rais Samia Suluhu Hassan anapenda wananchi wake waendelee na maisha ya Watanzania yabadilike watoke walipo na kusonga mbele na kupata maendeleo ya kweli” alisema.
Aliwataka Maafisa Maendeleo ya Jamii hao kwenda kwa kuwafundisha jinsi ya kuibua miradi ambayo itawasaidia wenyewe.
Katika hatua Nyingine wakazi wa Ifucha wamemuomba Mkuu wa Mkoa wa Tabora kuwafikisha kilio chao cha bei ya Mbolea kuwa juu kiasi kitachowafanya washindwe kulima.
Chiku Rashid alisema bei imepanda sana kutoka elfu 60 hadi laki moja jambo ambalo linaonekana ni mzigo kwao.
Said Haruna alisema kuwa udongo wa Tabora ni mchanga bila matumizi ya mbolea hakuna mavuno.
Balozi Dkt. Batilda alisema kilio chao atakifikisha kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa