Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, Dkt. John Mboya, amefungua kikao kazi cha Wakuu wa Idara za Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu kutoka halmashauri zote za mkoa wa Tabora, chenye lengo la kuboresha ufanisi wa utendaji katika utumishi wa umma. Kikao hicho kimefanyika katika ukumbi mdogo wa Ofisi ya Katibu Tawala wa Mkoa.
Akitoa neno la utangulizi, Katibu Tawala Msaidizi sehemu ya Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu, Bi. Upendo Joseph Haule, alisema kuwa madhumuni makuu ya kikao hicho ni kuimarisha utendaji kazi, kuongeza tija na kuhakikisha huduma bora zaidi zinatolewa kwa watumishi na wananchi wa mkoa wa Tabora.
Akizungumza wakati wa ufunguzi, Dkt. Mboya aliwapongeza wakuu wa idara hao kwa mchango wao mkubwa katika kusimamia rasilimali watu, na kusisitiza umuhimu wa kuendelea kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kujituma. Aliwataka watalaam hao kuhakikisha wanahudumia wananchi kwa weledi na nidhamu, ili kuendana na matarajio ya Serikali.
Dkt. Mboya alieleza kuwa Serikali inalenga kujenga utumishi wa umma uliotukuka na wenye maadili, unaozingatia sheria, taratibu na kanuni za kazi. “Tunahitaji kuona utumishi wa umma uliotukuka. Tunataka kuwa na watumishi wa umma ambao ni kioo cha jamii. Nendeni mkajenge mahusiano yenye afya na motisha mahala pa kazi,” alisisitiza.
Kwa upande wake, Bi. Haule alieleza kuwa kikao hicho kitajadili ajenda 12 muhimu zinazohusu masuala ya usimamizi wa rasilimali watu. Miongoni mwa mada zilizojadiliwa ni pamoja na usimamizi wa mfumo wa E-Utendaji, ufuatiliaji wa masuala ya kinidhamu kwa kuzingatia sheria, usafishaji wa taarifa za watumishi katika mifumo ya kielektroniki, mapitio ya mwongozo wa kujitolea kazini, pamoja na taratibu za uhamisho wa watumishi.
Aliongeza kuwa majadiliano hayo yanalenga kuleta maboresho ya kiutendaji, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha kuwa utumishi wa umma unakuwa na tija zaidi kwa maendeleo ya mkoa na taifa kwa ujumla.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa