Kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Katibu Tawala wa Mkoa huo, Dkt. John Mboya, amekutana na vijana wanaojishughulisha na biashara ya usafirishaji kwa kutumia pikipiki maarufu kama bodaboda, katika ofisi ya Mtendaji wa Kata ya Tabora Mjini, kwa lengo la kujadili masuala ya usalama na ustawi wa sekta hiyo.
Katika mkutano huo, Dkt. Mboya aliambatana na viongozi mbalimbali wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Tabora wakiwemo Mkuu wa Upelelezi na Makosa ya Jinai wa Mkoa,Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) Twaha Juma Lulengelule, Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Tabora, Mrakibu Mwandamizi wa Polisi (SSP) Peter Magayane, Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa ya Tabora, Dkt. John Pima pamoja na Afisa Maendeleo ya Jamii wa Mkoa, Bi. Monica Yesaya.
Akizungumza na bodaboda hao, Dkt. Mboya amewataka vijana kuepuka kabisa vitendo vya kujichukulia sheria mkononi, badala yake waachie vyombo vya dola vifanye kazi yake kwa mujibu wa sheria ili haki iweze kupatikana.
Amesema kufuatia matukio ya mauaji na uporaji wa pikipiki yaliyotokea hivi karibuni mkoani Tabora, Jeshi la Polisi limechukua hatua madhubuti kupitia vikosi kazi maalum vilivyoundwa kwa maelekezo ya Mkuu wa Mkoa, Mhe. Paulo Chacha, ambapo tayari watuhumiwa zaidi ya nane wamekamatwa na uchunguzi unaendelea.
“Hivyo niwaombe watoa huduma wa usafiri wa bodaboda kutoa ushirikiano wa karibu kwa Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya usalama ili mitandao ya uhalifu iweze kukomeshwa kwa mujibu wa sheria. Ushirikiano wa dhati utasaidia sana kurahisisha kazi za kiusalama,” alisisitiza Dkt. Mboya.
Aliongeza kuwa jukumu la Serikali ni kuhakikisha wananchi wanafanya kazi katika mazingira ya amani na utulivu bila vitisho wala bughudha, na pale panapotokea viashiria vya uvunjifu wa usalama, Serikali huchukua hatua za haraka kukabiliana navyo.
Kwa upande wake, Mkuu wa Upelelezi na Makosa ya Jinai wa Mkoa ACP Twaha Lulengelule , amewataka waendesha bodaboda kufanya kazi kwa tahadhari kubwa, hasa nyakati za usiku, kwani wahalifu wamekuwa wakitumia mbinu mbalimbali za udanganyifu. Pia amewasisitiza kuwa nadhifu na kuepuka mienendo na mavazi yasiyoendana na maadili ya Kitanzania.
Naye Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Tabora, SSP Peter Magayane, amewataka bodaboda kufuata sheria na taratibu za usafirishaji kama zilivyoainishwa katika Kanuni za Utoaji Leseni za Usafiri (Pikipiki na Bajaji), 2010 – Tangazo la Serikali Na. 144 la Mwaka 2010.
Amekemea vitendo vya uzembe barabarani ikiwemo kuendesha pikipiki kwa mwendo kasi, kufanya mashindano yasiyo rasmi pamoja na kutozingatia sheria za barabarani, mambo ambayo yamesababisha ajali nyingi zisizo za lazima.
“Sasa niwaombe muendeshe pikipiki sio pikipiki ziwaendeshe,” alisisitiza SSP Magayane.
Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Tabora, Bi. Monica Yesaya, amewahamasisha vijana wa bodaboda kutumia fursa mbalimbali za kiuchumi zinazotolewa na Serikali badala ya kuendelea kukopa pikipiki kwa masharti magumu. Amewataja baadhi ya fursa hizo kuwa ni mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri, mikopo yenye riba nafuu ya asilimia saba kupitia Benki ya NMB, pamoja na zabuni za Serikali kupitia PPRA ambapo asilimia 30 ya zabuni zimetengwa kwa makundi maalum ya vijana, wanawake na watu wenye ulemavu.
Akichangia hoja katika mkutano huo, Mwenyekiti wa Bodaboda Mkoa wa Tabora, Bw. Mrisho Hassan Shime, amelishukuru Jeshi la Polisi kwa ushirikiano wanaoutoa na kuomba uvumilivu pale makosa madogo yanapojitokeza, akiahidi kuwa bodaboda wengi kwa sasa wameelimika na wako tayari kufuata sheria na kanuni za usafirishaji.
Mkutano huo umeonekana kuwa chachu muhimu ya kuimarisha ushirikiano kati ya Serikali, Jeshi la Polisi na waendesha bodaboda mkoani Tabora kwa lengo la kujenga mazingira salama ya kazi na usafiri kwa wananchi wote.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa