Zaidi ya wanachama 420 kutoka vyama vya Msingi (AMCOS) Mkoani Tabora wamempongeza na kumshukuru Mhe, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuhakikisha wakulima wa Tumbaku wanapata Mbolea ya Ruzuku ya kutosha na kwa wakati pasipo na changamoto zozote kama ilivyokuwa hapo awali. Hayo yamejiri Leo Oktoba 6, 2023 wakati wa Ufungaji wa Mafunzo ya Wenyeviti na Watendaji wa AMCOS zilizopo Wilayani Urambo na Kaliua.
Naye, Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Burian, amewahakikishia wakulima wa Tumbaku kuwa, Serikali inatambua mchango wao na hivyo ina kila wajibu wa kuhakikisha wakulima hao wanapata mbolea ya ruzuku kwa wakati ili kukuza uzalishaji wa zao la Tumbaku.
“Serikali inatambua mchango wa wakulima wa Tumbaku, na tayari Mhe. Rais ameshatenga fedha kwa ajili ya mbolea ya ruzuku ambayo ipo tayari na kuwafikia wakulima wakati wowote, na nitoe wito kwa wakulima kujisajili kwenye mfumo uliowekwa kwa kufuata vigezo na taratibu” Alisema Dkt. Batilda
Sambamba na hilo , Dkt. Batilda ametoa wito kwa viongozi na watendaji wa AMCOS kuhakikisha wanawajibika kwa mujibu wa Sheria zilizowekwa ili kuendesha na kusimamia vyama vya msingi.
“Viongozi na Watendaji wote wa Vyama vya Ushirika mnaelekezwa kusimamia na kuendesha vyama vya Ushirika kwa kuzingatia sheria ya Vyama vya Ushirika Na. 6 ya mwaka 2013 ili kulinda maslahi ya wakulima wa Tumbaku” Alisisitiza Mkuu wa Mkoa
Aidha, Mhe, Mkuu wa Mkoa, ameeleza juhudi za Serikali ya awamu ya sita katika inapigania na kulinda maslahi ya wakulima wa Tumbaku kwa kuhakikisha wakulima wanapata malipo yao kwa wakati uliopangwa.
“Mpaka sasa kiasi cha fedha ambacho kimelipwa ni kiasi USD 141,168,519 na deni lililobaki mpaka sasa ni USD 3,563,832.6 ambapo tayari Serikali imeshatoa maelekezo mpaka kufikia tarehe 10 Oktoba, 2023 Kampuni zinazodaiwa ziwe zimeshalipa deni hilo.” Alisema Mhe. Mkuu wa Mkoa.
Mbali na hayo Mkuu wa Mkoa alitoa maelekezo kama, Halmashauri kukaa na kamati za Pembejeo na kufanya mapitio ya bei za mbolea, pia ameeleza mikakati ya Serikali ya kutafuta wadau wa Bima za mazao ili kupambana na majanga ya mvua za mawe ambazo huathiri tumbaku kwa kiasi kikubwa.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa