Serikali kupitia Ofisi ya Rais TAMISEMI imesema itawekeza katika kuhakikisha maafisa ustawi wa jamii katika halamshauri zote nchini wanapatiwa mafunzo ili kuwajengea maafisa hao uwezo wa kutekeleza majukumu yao ya kuhudumia wananchi.
Hayo yamesemwa leo Januari 31, 2024 Mkoani Tabora na Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Tabora Dkt. Ismail Kaponta wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya upangaji wa mipango na bajeti ya shughiri za ustawi wa jamii uliofanyika katika ukumbi wa Hotel ya Grand Penta, Manispaa ya Tabora.
Akitoa hotuba yake Dkt. Kaponta amesema kuwa mafunzo haya yana malengo ya kuwajengea uwezo maafisa ustawi wa jamii katika kutimiza majukumu yao hususani katika upangaji wa mipango na bajeti ambayo itasaidia kukamilisha adhma ya serikali katika kuhakikisha huduma za ustawi zinawafikia.
“Nipende kukumbushia kuwa malengo ya mafunzo haya ni kuwajengea uwezo nyinyi maafisa ustawi wa jamii ambao unakwenda kuwahudumia wananchi kwenye halmashauri zenu hususani kwenye upangaji wa mipango kwa kuzingatia bajeti” alisema Dkt. Kaponta
Aidha Dkt. Kaponta amewataka Maafisa Ustawi wa Jamii kote nchini kusimamia utekelezaji wa mipango mbalimbali ya maendeleo kwa kuzingatia sheria na miongozo inayopaswa kufuatwa katika kutoa huduma za ustawi wa jamii kwa jamii ili kupunguza matatizo yanayoweza kutokea kutokana kwenye jamii hizo.
Naye Mratibu wa Mipango na Bajeti Shughuri za Ustawi wa Jamii kutoka Ofisi ya Rais- TAMISEMI Bi. Zainabu Kitembe amekiri kuwepo na changamoto ya ufinyu wa bajeti kwa maafisa ustawi wa jamii katika kukamilisha majukumu yao ya kila siku jambo ambalo upelekea maafisa wengi kufanya kazi kwenye mazingira magumu.
“unakuta kuna wakati maafisa wa ustawi wa jamii wanafanya kazi kwa “stress” sana na wengi wao hawana furaha na kazi yao kutokana na kukosekana kwa bajeti ya kutekeleza majuku yao ya kuhudumia jamii” alisema Bi. Zainabu
Ameongeza kuwa, licha ya kuwa na changamoto ya ufinyu wa bajeti, bado serikali imeendelea kutambua mchango na nafasi ya maafisa hao kwenye ustawi wa jamii na sasa imetoa nafasi kwa maafisa hao kupata mafunzo haya ya upangaji wa mipango na bajeti ya shughuri ya ustawi wa jamii.
“tunatambua mchango wenu kwenye ustawi wa jamii, na tulitamani maafisa wote wa ustawi wa jamii wahudhurie mafunzo haya lakini kutokana na bajeti mmekuja wachache” aliongeza Bi. Zainabu.
Kwa upande wa Mwakilishi wa Shirika la PACT Tanzania Bi. Flora Nyagawa amesema kuwa, PACT imetoa mchango mkubwa wa uanzishwaji wa mafunzo ya mfumo wa upangaji wa mipango na bajeti ya ustawi wa jamii na sasa hivi wameendelea kufadhiri mafunzo haya kwa maafista wa ustawi wa jamii na watalaamu wengine wanahusika na shughuri za ustwawi wa jamii.
Mafunzo haya ya mfumo wa upangaji wa mipango na bajeti ya shughuri za ustawi wa jamii yalioanza Januari 29, 2024, yanahusisha maafisa ustawi wa jamii, maafisa mipango, waganga wakuu na makatibu wa afya kutoka halmashauri mbalimbali nchini.yamefadhiliwa na shirika la kimataifa la PACT Tanzania kupitia mradi wake wa ARCHIVE unaohusika na kusaidia Watoto wanaoishi mazingira hatarishi.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa