Kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Dkt John Mboya Katibu Tawala Mkoa wa Tabora ametembelea maeneo yalioathiriwa na mvua zinaendelea kunyesha Manispaa ya Tabora, Mkoani Tabora kwa kutembelea Kata ya Malolo na Mpera na kujionea hali halisi leo Januari 29, 2024.
Dkt. John Mboya amewataka wakazi wa Mkoa wa Tabora kuhama maeneo yote ambayo hujaa maji pindi mvua zinaponyesha ili kuepukana na madhara yanayosababishwa na mvua hizo.
“kama serikali napenda kutoa maagizo kwa wananchi wanaoishi maeneo ambayo maji hujaa pindi mvua inaponyesha ili kuepukana na madhara yanayoweza kusababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha ikiwemo vifo na upotevu wa mali.” Alisema Dkt. Mboya
Dkt. Mboya ameongeza kuwa, Serikali yetu ipo macho wakati wote na ikumbukwe kuwa, hapo awali Serikali kwa kushirikiana na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), ilishatoa tahadhari kuhusiana na mvua zinazoendelea kunyesha sasa.
Aidha Dkt. John Mboya amewapongeza watendaji wote wa TARURA na TANROAD kwa kuhakikisha wanachukua hatua za haraka licha ya ugumu wa kufika baadhi ya maeneo ambayo yameathiriwa na mvua zinazoendelea kunyesha mpaka sasa.
Naye, Diwani wa Kata ya Mpera Mhe. Haruna Msoga amesema kuwa, mpaka sasa hakuna maafa yaliotokea hususani vifo na nyumba kubomoka licha ya nyumba nyingi kuzingilwa na maji kutokana na mvua iliyonyesha asubuhi ya leo.
Kwa upande mwingine Diwani wa Kata ya Malolo Mhe. Zinduna Kambangwa ameiomba Serikali kuhimarisha miundombinu ambayo tayari imeshajengwa ili kuhakikisha miundombinu hiyo inazuia maji kusambaa kwenye makazi ya watu.
Naye. Meneja wa TARURA Wilaya ya Tabora Muhandisi Subira Vicent Manyama amesema, ni kweli tumeona maji yameleta athari kwa wananchi na sisi kama TARURA tulishachukua hatua kwa kuleta mtambo wa kutengeneza barabara, lakini kutokana na hali ilivyo ilishindikana na kusitisha zoezi hilo, na sisi kama TARURA mpango uliopo ni kujenga kingo ambazo zitazuia maji kusambaa kwa watu.
Meneja wa TARURA Mkoa wa Tabora Muhandisi Lusako Kilembe amesema kuwa , Changamoto ya mitaro tayari tumeshatafuta suluhisho la kudumu na tayari serikali kupitia wizara ya TAMISEMI imeshaanza kupokea maoni kutoka kwa mameneja wa TARURA ili kukabiliana na changamoto hii. Lakini kwa sasa tumeshaanza kuyaondoa maji haya kama moja ya hatua za awali ili kuzuia maji kusambaa kwenye makazi ya watu.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa