MKUU wa Mkoa wa Tabora Dkt. Philemon Sengati amekabidhi hundi yenye thamani shilingi milioni 142 kwa vikundi 29 vya wanawake na vijana wa Manispaa ya Tabora.
Mikopo imetolewa kwa vikundi hivyo ikiwa ni sehemu ya Manispaa ya Tabora kutimiza takwa la Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa yam waka 2019 ya kutengwa kwa asilimia 10 kwa ajili ya wanawake, vijana na walemavu.
Dkt. Sengati amekabidhi mikopo hiyo katika hafla fupi iliyofanyika katika Viwanja vya nane nane.
Alivitaka vikundi vilivyokabidhi kutumia fedha hizo katika miradi na malengo waliyoombea mikopo na sio katika shughuli nyingine zisizokuwa za maendeleo.
Dkt. Sengati aliutaka Uongozi wa Manispaa kuandaa mpango wa kutoa elimu ya usimamizi wa fedha na kufikiri kimkakati kwa wajasiriamali kabla ya kuwapa mikopo ili waweze kutumia fedha hizo kwa ajili ya kujiletea maendeleo.
Aidha Mkuu huyo wa Mkoa aliutaka uongozi wa Manispaa ya Tabora kutoa mikopo kwa uwazi bila ucheleweshaji na rushwa kwa vikundi vinavyoomba.
Dkt. Sengati aliongeza sanjari hilo ni fedha wakatoa fedha nyingi na vifaa kwa vikundi ili matokeo yake yaweze kuleta tija kwao na Mkoa kwa ujumla.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora Christina Bunini alisema katika mwaka wa fedha unaoendelea wametenga kiasi cha shilingi milioni 445.1 kwa ajili mikopo ya vikundi kama sheria inavyotaka.
Alisema kati ya fedha hizo wamepanga kutoa kiasi cha shilingi milioni 178 kwa wanawake, milioni 178 kwa vijana na milioni 89 kwa watu wenye ulemavu.
Bunini aliongeza hadi hivi wameshapokea maombi mengi zaidi ya fedha ya fedha iliyotengwa katika bajeti.
Alisema toka Julai hadi Oktoba mwaka huu wameshapokea maombi ya mikopo kwa vikundi 79 ambayo thamani yake ni sawa na shilingi milioni 566.5.
Bunini alisema kati ya fedha hizo vikundi 61 vya wanawake vimeomba kiasi cha shilingi milioni 463, vijana 12 vimeomba shilingi 76 na watu wenye ulemavu 6 vimeomba shilingi milioni 27.
Naye Afisa Maendeleo ya Jamii Manispaa ya Tabora Tumaini Mgaya alisema hadi hivi sasa Manispaa ya Tabora imekwisha kutoa kiasi cha shilingi milioni 211 kwa vikundi 41.
Alisema kuwa pamoja na jitihada hizo kuna baadhi ya vikundi vimekuwa havirejeshi mikopo kwa wakati na kusababisha wanavikundi wengine wanaohitaji kuchelewa kupata fedha.
Alisema miongoni mwa vikundi ambavyo vinadaiwa ni vya vijana na watu wenye ulemavu na kuna baadhi ya vikundi vimekuwa vikianzisha miradi tofauti na ile waliyombea mikopo.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa