Na. OMM Tabora.
Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mheshimiwa Paulo Chacha, ameongoza oparesheni maalum ya kuteketeza shamba kubwa la bangi lililolimwa ndani ya Msitu wa Hifadhi wa Nyahua Mbuga, wilayani Sikonge. Shamba hilo linakadiriwa kuwa na ukubwa wa ekari 3 na eneo la hifadhi hiyo lina ukubwa wa hekta 679,000, hatua ambayo imeibua taharuki na mshangao kutokana na kiwango kikubwa cha uvunjifu wa sheria.
Oparesheni hiyo ilihusisha Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Tabora, Kamati ya Ulinzi ya Wilaya ya Sikonge pamoja na watendaji wa serikali kutoka ngazi ya mkoa na wilaya. Hatua hiyo imechukuliwa kufuatia taarifa za kiintelijensia zilizowasilishwa na vyombo vya usalama kuhusu uwepo wa kilimo haramu katika eneo la hifadhi.
Akizungumza mara baada ya tukio hilo, Mhe. Chacha alionesha masikitiko makubwa juu ya kitendo cha baadhi ya wananchi kuamua kwa makusudi kuingia maeneo ya hifadhi kinyume na sheria, kisha kuendesha shughuli haramu za kilimo cha bangi.
“Haiwezekani tukavumilia uhalifu wa waziwazi kama huu. Sheria lazima ifuate mkondo wake. Tunatoa onyo kali kwa wote wanaojihusisha na kilimo hiki haramu, wasitafute kuhalalisha uovu katika maeneo ya hifadhi,” alisisitiza Mhe. Chacha.
Aidha, alitoa wito kwa wananchi wote wa mkoa wa Tabora na maeneo jirani kuacha mara moja tabia ya kuingia katika maeneo ya hifadhi kwa shughuli yoyote ile bila kibali, akisisitiza kuwa Serikali haitasita kuchukua hatua kali kwa yeyote atakayebainika kuvunja sheria.
Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, SACP Richard Abwao, alisema kuwa uchunguzi wa kina unaendelea ili kubaini watu wote waliohusika katika kilimo hicho haramu.
Tukio hili linakuja wakati ambapo juhudi za serikali za kupambana na uhalifu wa mazingira na dawa za kulevya zimeongezwa, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kitaifa wa kulinda rasilimali na kuhakikisha ustawi wa wananchi.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa