Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Burian ameridhishwa na usimamizi wa miradi inayotekelezwa ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Nzega ikiwemo mradi wa ujenzi wa makao makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Nzega sambamba na mradi wa ujenzi wa Hospitali mpya ya Wilaya. Ameyasema hayo leo Februari 14, 2024 alipofanya ziara yake wilayani Nzega na kujionea maendeleo ya miradi hiyo.
Mhe. Mkuu wa Mkoa amewapongeza wasimamizi wa miradi hiyo ambayo kwa hakika imeonyesha thamani ya fedha za serikali kwa kiasi kikubwa na kwamba kukamilika kwa majengo hayo kutaongeza imani kwa wananchi juu ya utendaji kazi wa watumishi wa serikali wilayani humo.
“nipende kutoa pongezi zangu kwa wote waliosimamia miradi hii ambayo inakwenda kuongoza imani kwa wananchi kwa kuwa wanapata huduma pasipo kusafiri umbali mrefu” alisema Mhe. Mkuu wa Mkoa.
Sambamba na hilo, Mhe. Batilda ametoa wito kwa mkurugenzi na timu yake kubuni miradi mbalimbali ya maendeleo ili kuchangamkia fursa mbalimbali zilizopo maeneo hayo kutokana na uwepo wa makao makuu ya halmashauri hiyo.
“nitoe wito kwa mkurugenzi na watendaji wako kuhakikisha mnabuni vyanzo mbalimbali vya mapato na katumia fursa mbalimbali zilizopo kutokana na uwepo wa ofisi hii ambayo ina wafanyakazi ambao watahitaji huduma mbalimbali” alisema Mhe. Batilda
Aidha Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa ametoa muda wa wiki mbili kwa ajili kufanya marekebisho madogo madogo yaliopo katika baadhi ya majengo na kutoa wito kwa wasimamizi kufanya marekebisho hayo pasipo kusubiri viongozi wafike.
“msisubiri mpaka sisi tuje hapa ndio tutoe maelekezo ya kufanya marekebisho, na hivyo natoa wiki mbili za kufanya marekebisho yote ambayo yamejitokeza kwenye majengo yote” alisema Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa
Naye Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nzega Muhandisi Modest Apolinary ameeleza umuhimu wa kukamilika kwa miradi hiyo ikiwemo kusogeza na kuboresha huduma kwa jamii sambamba na kuweka mazingira mazuri kwa watendaji kuwahudumia wananchi.
Kwa upande wa Muhandisi kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora, Muhandisi Faustine Talai amemuhakikishia mkuu wa mkoa kusimamia na kutekeleza maagizo na mapendekezo yote yaliotolewa na kukamilisha miradi yote kwa wakati na kwa viwango vinavyotakiwa.
Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Burian alifika wilayani Nzega na kutembelea mradi wa makao makuu ya halmashauri ya wilaya ya Nzega pamoja na majengo mapya ya Hospitali ya Wilaya ya Nzega ambapo ameridhishwa na kasi ya utekelezaji wa miradi hiyo ambapo Halmashauri ya Wilaya ya Nzega ilipokea fedha kwa awamu 3 kwa ajili ya ujenzi wa jengo hilo, katika mwaka wa Fedha 2020/2021 kiasi cha Tsh. 1,000,000,000, mwaka wa fedha 2021/2022 ilipokea tena kiasi cha Tsh. 1,000,000,000 na mwaka 2022/2023 ilipokea Tsh. 1,000,000,000 na kupelekea Jumla ya Fedha za Ujenzi wa Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Nzega kuwa Tsh. 3,000,000,000 (Bilioni tatu tu) kutoka Serikali kuu.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa