Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Burian amewataka wasimamizi wa shule zinazojengwa na kuboreshwa kupitia fedha za miradi ya BOOST, wanafanya kazi usiku na mchana kukamilisha miradi hiyo kabla ya Julai 20, mwaka huu. “Tuhakikishe tunafanya kazi usiku na mchana kama tulivyokubaliana, muda uliobaki ni mchache na fedha zilichelewa kuingia lakini sisi siku zote hatutafutagi sababu na hivyo hatuna sababu ya miradi hii kutokukamilika kwa wakati”. Alisema
Aidha Dkt. Batilda amewataka watendaji wa Serikali kufuata taratibu nzuri za malipo kwa mafundi na wakandarasi pasipo kupoteza muda wa malipo hayo, kwani Serikali ilishatoa fedha kwa ajili ya kukamilisha miradi hiyo. “Tunawaombeni sana kazi inapofanyika mafundi walipwe fedha zao kwa wakati, hatutaki kusikia baadae kuna watu wanadai” alisema Mkuu wa Mkoa.
Kwa upande mwingine amewapongeza baadhi ya wakinamama waliokuwa wanafanya kazi ya umwagaji zega katika miradi hiyo na kwamba Mhe.Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anatambua nafasi ya wanawake katika ukamilishwaji wa miradi ya Serikali.“Nimefurahishwa sana kuwakuta wakinamama wajenzi katika mradi huu, imenipa moyo na amasa kubwa” Alisema Dkt. Batilda
Kupitia Program ya BOOST, Mkoa wa Tabora umepata jumla ya shilingi Bilioni 12.1 kwa ajili ya ujenzi wa shule za msingi mpya 17, vyumba vya madarasa 118, vyumba vya madarasa ya mfano ya Elimu ya Awali 16, matundu ya vyoo 130 na nyumba za walimu 2 (2 in 1). Fedha hizo tayari zimepokelewa katika shule husika tayari kwa kuanza utekelezaji wake.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa