NA TIGANYA VINCENT
WANAWAKE Mkoani Tabora wametakiwa kujihusisha na ufugaji wa kuku ili kujiongezea kipato kwa ajili ya maendeleo yao na familia zao.
Kauli hiyo imetolewa leo na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Balozi Dkt Batilda Buriani wakati akifungua mafunzo kwa Madiwani wa Viti maalumu na wanawake ambao wanaongoza Kata yaliyoandaliwa na Mbunge wa Viti Maalum Mkoa Mkuu wa Tabora Munde Tambwe.
Alisema kuwa uwepo wa miradi mikubwa inayotekeleza kama vile ujenzi wa Bomba la Mafuta kutoka Uganda hadi Tanzania ni fursa kwao kuuza bidhaa mbalimbali.
Balozi Dkt. Batilda aliwataka kutumia mafunzo ya ufugaji wa kuku kuboresha ufugaji ili waweze kuleta mapinduzi ya kimaendeleo kutokana na uuzaji wa kuku.
Alisema sio vizuri kuagiza kuku kutoka nje ya Mkoa wa Tabora wakati maeneo mazuri ya ufugaji yapo.
Katika hatua nyingine Mkuu huyo wa Mkoa alimpongeza Munde kwa kuhakikisha anatoa msaada wa majigo ya gesi kwa wanawake ambao unalenga kutunza mazingira
Awali Munde alisema kuwa ameandaa mafunzo ambayo yanalenga kuwajengea uwezo wanawake katika ufugaji wa kuku, kilimo bora cha Alizeti ili baadaye awape mtaji ambao watatumia kujiendeleza wenyewe.
Alisema baada ya mafunzo hayo atatoa shilingi laki mbili kwa kila Kata kwa ajili ya wanawake kuanzisha mradi wa ufugaji kuku ambao baada ya kuongezeka watasambaza kwa wanawake wengine bila kujali ili kadi ili nao wajiendeleza.
Munde alisema kwa upande wa kilimo atawekeza kwa wanawake kwa kutoa mbegu za alizeti ya shilingi milioni 6 kwa kila Wilaya ya Mkoa wa Tabora ambazo zitagharimu milioni 52.
Aidha alisema katika kuhakikisha kuwa wanawake hawatumii muda mwingi kutafuta kuni kwa ajili ya kupikia atatoa majiko ya gesi 670 yenye thamani ya milioni 30.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa