Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Burian, amemuagiza Mkuu wa Wilaya Urambo Mhe. Eribariki Bajuta kwenda kufanya kazi na kuwatumikia wanaurambo kwani Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amemuamini na kumpatia nafasi hiyo. Ameyasema hayo leo Oktoba 4, 2023 alipokuwa akimuapisha Mkuu wa Wilaya huyo kwenye Ukumbi wa Isike Mwanakiyungi.
Sambamba na hilo, Mkuu wa Mkoa amemtaka DC. Bajuta kusimamia amani ambayo ni tunu kwa Watanzania na Urambo kwa ujumla ili kuhakikisha wananchi wanapata nafasi ya kushiriki kwenye shughuli za maendeleo.
“Ukiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Usalama ya Wilaya, hakikisha unasimamia Amani na Utulivu katika Wilaya yako ili wananchi wapate fursa ya kujishughulisha na kazi za maendelo ili wapate vipato na kupunguza umasikini” Alisema Mhe. Batilda
Pia amemuagiza Mkuu wa Wilaya wa Urambo kwenda kusimamia maslahi ya wakulima hususani suala zima la madeni ambayo yamekuwa kero kwa wakulima wa zao la Tumbaku Wilayani Urambo.
“Wananchi wa Wilaya ya Urambo ni wakulima wa mazao ya Chakula na Mazao ya biashara hususani Kilimo cha Tumbaku, hivyo ukasimamie kuhakikisha Madeni ya wakulima wa Tumbaku yanalipwa na Vyama vya Ushirika” alisisitiza Mkuu wa Mkoa.
Aidha Dkt. Batilda amemuagiza DC. Eribariki Bajuta kushirikiana na watendaji wa serikali wa ngazi zote ili kuhakikisha wanawatumikia wananchi wa Urambo ambao wanategemea kwa kiasi kikubwa miradi ya maendeleo inayoletwa na Serikali.
“Kasimamie Mamlaka za Serikali za Mitaa (Halmashauri) ili iwatumikie wananchi kwani Halmshauri zinapewa fedha nyingi za kukamilisha miradi mbalimbali ya maendeleo ili kuhakikisha huduma bora zinatolewa kwa wananchi” Alisema Dkt. Batilda
Mbali ya hayo Mhe. Mkuu wa Mkoa alimuagiza Mkuu wa Wilaya ya Urambo kusimamia mambo kadha wa akdha yakiwemo, suala la utunzaji wa mazingira, kufanya mikutano ili kuwasikiliza na kutatua kero za wananchi na pia kuendeleza baadhi ya mambo yaliokuwa yakifanywa na mtangulizi wake.
Mhe. Eribariki Saimon Bajuta anakwenda kuwa Mkuu wa Wilaya ya Urambo, kuchukua nafasi ya Mhe. Kenani Kihongosi ambaye anakwenda kuwa Mkuu wa Wilaya ya Momba, Mkoani Songwe.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa