Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mh. Balozi Dkt. Batilda Salha Burian amemshukuru Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutenga shilingi Bilioni 8.6 kwa ajili ya rukuzu ya mbolea ambayo kwa hakika imewapunguzia mzigo wakulima kwa asilimia 44. Ameyasema haya leo alipohutubia mamia ya wananchi waliofika kwenye kilele cha Maadhimisho Ya Siku Ya Mbolea Duniani kwenye viwanja vya Chipukizi, Manispaa ya Tabora.
“Serikali imeendelea kutoa ruzuku ya pembejeo ambapo katika msimu wa kilimo wa 2022/23, Mkoa wa Tabora umepokea Tani 8 za mbolea ya ruzuku yenye thamani ya Shilingi Bilioni 19.5. Kati ya hizo, shilingi Bilioni 10.9 zilitolewa na wakulima. Ruzuku ya Serikali ilikuwa ni shilingi Bilioni 8.6 Ruzuku hiyo imewapunguzia wakulima mzigo wa kununua mbolea kwa asilimia 44” Alisema RC. Batilda
Mkuu wa Mkoa ameeleza kuwa, kufuatia uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali ya awamu ya sita, kasi ya uzalishaji wa mazao imeongezeka kutoka tani laki 9 mwaka 2021/2023 na kufikia tani milioni 1 kwa mwaka 2022/2023 sawa na ongezeko la asilimia 18.
“Kutokana na kazi kubwa inayofanywa na Serikali ya Awamu ya sita ya kutoa ruzuku ya pembejeo na vitendea kazi kwa maafisa ugani, uzalishaji wa mazao ya chakula katika Mkoa wa Tabora umeongezeka kutoka tani laki 9 mwaka 2021/2022 hadi tani milioni 1 mwaka 2022/2022. Ongezeko hilo ni sawa na asilimia 18.6.” alisisitiza Mkuu wa Mkoa.
Mkuu wa Mkoa ameeleza kuwa, mpaka sasa Mkoa umeshaweka mikakati ya kuhakikisha zoezi zima la usambazaji wa mbolea kwa wakulima linafanikiwa kwa kushirikiana na watendaji wa Wilaya na Halmashauri zote na Mkoa unatarajia kuwa na vituo 80 vya kuuzia licha ya sasa kuwa na vituo 27.
“Msimu huu, Mkoa umejipanga vizuri kuhakikisha kila Wilaya inakuwa na vituo vya kutosha vya uuzaji wa mbolea. Kwa sasa tuna jumla ya vituo 27 vya kuuzia mbolea. Matarajio yetu kabla ya msimu wa kilimo kuanza tutakuwa na jumla ya vituo 80” Alisema Mkuu wa Mkoa.
Kufuatia ujio wa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuria wa Tanzania, Mkoani Tabora, Mhe. Mkuu wa Mkoa ametoa wito kwa wananchi wa Tabora kujitokeza kwa wingi kwenye mapokezi ya Mhe. Rais ambaye anatarajiwa kufanya ziara yake hapa Mkoani Tabora.
“Kama mnavyojua Mkoa wetu umepata bahati ya ujio wa Mheshimiwa Rais, ambaye anatarajiwa kuja hapa Mkoani kwetu. Na hivyo niwaombe mjitokeze kwa wingi kumpokea Rais wetu mpendwa” Alisema Mhe. Mkuu wa Mkoa.
Maadhimisho ya Siku ya Mbolea Duniani yalizinduliwa rasmi mnamo Oktoba 11, 2023 na kuhitimishwa leo Oktoba 13, 2023 yenye kauli mbiu isemayo “Matumizi sahihi ya mbolea ya ruzuku, kwa kilimo chenye tija”
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa