Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Burian amewataka wakazi wa Tabora na Kigoma kutumia maonesho ya Siku ya Wakulima (Nanenane) kama sehemu muhimu ya kujifunza shughuli mbalimbali za kimaendeleo. Ameyasema hayo leo Agosti 1, 2023 alipofanya mahojiano na waandishi wa habari ofisini kwake.
“Maonesho ya haya ni sehemu nzuri ya kujifunzia kwa kuona hali halisi ya wakulima, wafugaji na wavuvi wakipata fursa ya kujifunza teknolojia zinazosaidia kuongeza tija, uzalishaji na thamani ya mazao na bidhaa wanazozalisha” alisema Mkuu wa Mkoa wa Tabora.
Aidha, Dkt. Batilda Burian ametoa wito kwa wananchi wa Tabora na Kigoma kujitokeza kwa wingi kwenye viwanja vya Ipuli Manispaa ya Tabora kujionea shughuli mbalimbali za kilimo kipitia maonesho ya Nanenane.
“Kupitia vyombo vya habari, nawakaribisha wananchi wa Mikoa ya Tabora na Kigoma na Umma wa watanzania kwa ujumla kuhudhuria maadhimisho na maonesho hayo ambayo yameanza leo Jumanne tarehe 1 Agosti 2023 na yatafikia kilele tarehe 08 Agosti 2023” alisisitiza
Maadhimisho na Sherehe za Wakulima (Nane Nane) hufanyika kuanzia tarehe 1 hadi 8 mwezi Agosti kila mwaka. Kitaifa maadhimisho haya yanafanyika katika viwanja vya John Mwakangale Manispaa ya Mbeya. Aidha, maadhimisho hayo yanafanyika pia katika Kanda zote ikiwemo Kanda ya Magharibi inayojumuisha Mkoa wa Tabora na Kigoma. Kwa Kanda ya Magharibi maadhimisho yanafanyika katika viwanja vilivyoko Ipuli katika Manisapaa ya Tabora.
Kaulimbiu ya Nane nane mwaka 2023 ni “VIJANA NA WANAWAKE NI MSINGI IMARA WA MIFUMO ENDELEVU YA CHAKULA”.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa