Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Balozi Dkt Batilda Salha Burian amewataka Wakulima Mkoani Tabora kujitokeza na kwenda kujiandikisha na pia kurekebisha taarifa zao ili kuhakikisha Serikali inapata taarifa sahihi za wakulima wakati wa utoaji wa ruzuku za mbolea. Ameyasema hayo leo Julai 22, 2023 alipofanya mazungumzo na bodi ya uthibiti wa mbolea (TFRA) ofisini kwake.
“Basi mimi nawashauri kila mmoja aende akarekebishe taarifa zake na wala ambao hawajajiandikisha waende wakajiandikishe wapate namba kwa ajili ya Ruzuku” alisema
Sambamba na hilo, Dkt Batilda ameihakikishia bodi hiyo kuwa, Mkoa wa Tabora umejipanga kuhakikisha kilimo kinasonga mbele hususani kilimo cha tumbaku ambacho ndio zao kuu Mkoani Tabora.
“Sisi tumejianda vizuri na kama tunavyojua kilimo chetu kikubwa ni tumbaku na tuna mapendekezo mengi kutoka kwa wakulima wa tumbaku kuhusiana na ruzuku ya mbolea ambayo Serikali kwa kushirikiana na wadau tunayafanyia kazi” alisisitiza Mkuu wa Mkoa.
Aidha, Dkt. Batilda Burian amempongeza Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuzidi kuiamini Bodi hiyo na kuahidi kutoa ushirikiano ili kuhakikisha wakulima Mkoani Tabora wanapata mbolea kwa wakati.
Mapema Leo Julai 22, 2023 Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Balozi Dkt Batilda Salha Burian alikutana na kufanya mazungumzo na Wajumbe wa Bodi ya Uthibiti wa Mbolea ( TFRA) inayoongozwa na Mwenyekiti wake Dkt. Antony Diallo.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa