Katika kuhakikisha Mkoa wa Tabora unakwenda sambamba na kauli mbiu ya “Zero Maralia” Mkuu wa Wilaya ya Tabora Mhe. Louis Peter Bura akimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Burian, amewataka Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi kusimamia zoezi la ugawaji wa vyandarua litakapoanza ili kuhakikisha walengwa wote wanafikiwa. Ameyasema hayo leo Septemba 25, 2023 kwenye Kikao cha Uzinduzi wa Usambazaji wa Vyandarua kwenye Kaya, Mkoani Tabora.
“Nitoe maelekezo kwa wakuu wa Wilaya na wakurugenzi kuweka mikakati na kusimamia vizuri zoezi la ugawaji wa vyandarua katika kaya na kuweza kuwafikia walengwa kama ilivyokusudiwa na Serikali ili kupunguza maambukizi ya ugonjwa wa Malaria” Alisema Mhe. Bura.
Sambamba na hilo amewataka wataalamu wa masuala ya afya, kuwashirikisha viongozi wa kisiasa, dini pamoja na ngazi zote za kiserikali, kuhakikisha mapambano dhidi ya maralia yanakuwa suala la Jamii nzima na la kudumu.
“Pia nitoe wito kwa wataalamu wa Afya kuwashirikisha viongozi wa Siasa, dini na Serikali ngazi zote katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Malaria, ili mapambano dhidi ya ugonjwa huu iwe ajenda ya kudumu katika Vikao vyote vya Kisheria katika Wilaya na Halmashauri”
Aidha, Mhe. Bura ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kugawa vyandarua na kuongeza kasi kwa wananchi kupambana na Malaraia.
“Naishukuru sana Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kuratibu zoezi zima la upatikanaji wa vyandarua na kuongeza wigo kwa wananchi wa kupatiwa vyandarua hivyo ili kudhibiti ugonjwa wa Malaria”
Kwa mujibu wa Takwimu, Kiwango cha maambukizi ya Malaria katika Mkoa wa Tabora kwa watoto kati ya umri wa miezi 6 - 59 kimeongezeka kutoka 11.7% mwaka 2017/2018 hadi kufikia 23.4%, ikiwa kiwango cha maambikizi ya Malaria Kitaifa ni 8.1%. Hivyo Mkoa wa Tabora una kila sababu ya kuhakikisha zoezi la ugawaji wa vyandarua kwa kila kaya linawafikia watu wote ili kukabiliana na ugonjwa wa Maralia.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa