Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Burian amemshukuru Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kutenga fedha zaidi ya Bilioni 8.6 , kwa ajili ya ruzuku ya mbolea ambayo itakwenda kufaidisha wakulima zaidi ya elfu 29 Mkoani Tabora. Ameyasema hayo leo Oktoba, 8, 2023 alipofanya mkutano na waandishi wa Habari Ofisini kwake.
Mhe. Batilda Burian ameeleza kuwa, kupitia utolewaji wa fedha bilioni 8.6, Mkoa ulifanikia kupata Mbolea za aina mbalimbali tani elfu 8.2 ambayo tayari zimeshaanzwa kuwafikia wakulima elfu 29.5.
“Mkoa wa Tabora kupitia ruzuku hiyo ilitumia tani elfu 8.2 za mbolea mbalimbali zenye ruzuku ya Serikali bilioni 8.5 ambapo jumla ya wakulima 29,517 walinufaika na mbolea hiyo.” Alisema Mhe. Mkuu wa Mkoa.
Katika kuhakikisha wakulima wanafaidika na mbolea za ruzuku, Mkuu wa Mkoa ametoa wito kwa wakulima wote Mkoani Tabora kwenda kujisajili kwenye mfumo maalumu uliowekwa na Serikali ili kuhakikisha kila mkulima anapata mbolea hiyo ambayo Serikali imewekeza fedha nyingi.
“Niwaombe wakulima wa Mkoa wa Tabora kwenda kwenye Ofisi za Vijiji na Mitaa wakiwa na Vitambulisho vya Taifa (NIDA) au Mpiga Kura kwa ajili ya kujiandikisha kwenye vitabu vya usajili na wale waliojiandikisha mwaka jana kuhuisha taarifa zao ili waweze kunufaika na mpango wa mbolea ya ruzuku” Alisisitiza Mhe. Batilda.
Sambamba na hilo Mhe. Dkt Batilda Burian ametoa wito kwa wakulima wote Mkoani Tabora pamoja na mikoa ya jirani kujitokeza kwenye maadhimisho ya Siku ya Mbolea Duniani yatakayofanyika Mkoani Tabora, na kwamba maadhimisho hayo yanalenga kuwanufaisha wakulima wote hasa upande wa teknolojia na elimu juu ya matumizi sahihi ya mbolea.
“nitumie fursa hii kuwaalika na kuwakaribisha wakulima na wadau wa sekta ya kilimo kuja kujifunza teknologia mbalimbali za matumizi sahihi ya mbolea, afya ya udongo, viuatilifu na mbegu bora ili wakulima waweze kuzalisha tija”
Maadhimisho ya Siku ya Mbolea Duniani, kwa ngazi ya Taifa yatafanyikia Mkoani Tabora kwenye viwanja vya Chipukizi, Manispaa ya Tabora kuanzia Oktoba 11, 2023 hadi Oktoba 13, 2023. Kauli mbiu ya mwaka huu inasema “Matumizi Sahihi ya Mbolea ya Ruzuku kwa Kilimo chenye Tija”.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa