Mjasiriamali kutoka Tanzania ameibuka mshindi wa kwanza wa jumla kwenye Maonesho ya 23 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati ya Jumuiya ya Afrika Mashariki maarufu kama Nguvu Kazi/Juakali yaliyomalizika jijini Bujumbura, Burundi leo tarehe 15 Desemba 2023, Mshindi wa pili ametokea Kenya huku mshindi wa tatu akitokea Uganda.
Mjasiriamali huyo, Dkt. Herieth Mkanga anayejishughulisha na utengenezaji wa Batiki ameibuka mshindi kwa kutengeneza vazi maarufu la “Suti ya Samia” ikiashiria mtindo wa nguo unaopendelewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Akizungumza mara baada ya kupokea tuzo hiyo, Dkt. Mkanga amesema kuwa amefurahia ushindi huo ambao ni mkubwa kwake na kwa Tanzania na kwamba tuzo hiyo ni chachu kwake ya kuendelea kujituma zaidi na kutengeneza bidhaa nyingi na zenye ubora ili kulikamata soko la Afrika Mashariki, Afrika na Duniani kwa ujumla.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Ukuzaji Ajira, Bi. Kissa Kilindu amewahamasisha wajasiriamali kote nchini kujiamini na kuchangamkia fursa mbalimbali za biashara, masoko na uwekezaji zinazotangazwa na Serikali ndani na nje ya nchi.
Wakati huo huo kwa ngazi ya Taifa Mkoa wa Tabora umeibuka Mshindi wa Tatu (3) Kwa kuwa na Bidhaa zenye Ubora zinazozalishwa na Mjasiriamali Mwanahamis Rashidi mtengenezaji wa majiko kutoka kikundi cha Tabora Green Gurd.
Tunzo hizo zilitolea kwa kila nchi ambapo kwa Tanzania Mshindi wa Tatu alitokea Mkoani Tabora, mshindi wa Pili alitokea Mkoani Pwani na Mshindi wa Kwanza alitokea Mkoa wa Morogoro.
Ikumbukwe kuwa, Kwa mwaka huu Wajasiriamali zaidi ya arobaini (40) kutoka kwenye Wilaya zote za Mkoa wa Tabora wameshiriki kwenye maonesho hayo ya 23 ya Wajasiriamali Wadogo na wa Kati wa Jumuiya ya Afrika Mashariki maarufu Nguvu Kazi au Jua Kali yaliofanyika mjini Bujumbura, Burundi kuanzia Disemba 5, 2023 na kuhitimishwa leo Disemba 15, 2023, yaliokuwa na Kaulimbiu isemayo “Kuunganisha Wajasiriamali Wadogo na wa Kati wa Afrika Mashariki kufanya biashara katika Eneo la Afrika Mashariki” hufanyika kila mwaka kwa utaratibu wa mzunguko kutoka nchi moja kwenda nchi nyingine ambapo maonesho ya 24 yanatarajiwa kufanyika nchini Sudan Kusini mwaka 2024.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa