Mkuu wa Mkoa wa Tabora Mhe. Balozi Dkt. Batilda Salha Burian amewataka Wakurugenzi wa Halmashauri katika Wilaya zote za mkoa huo kutenga fedha kwa ajili ya sekta ya ardhi katika bajeti ya mwaka 2024/25 ili kuendeleza utekelezaji katika maeneo yale ambayo Mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi (LTIP) hautekelezwi.
Mhe. Mkuu wa Mkoa amesema wadau wa ardhi mkoa wa Tabora watumie fursa kujadili namna bora ya kutekeleza Mradi wa Uboreshaji Usalama wa Milki za Ardhi (LTIP) katika maeneo yao wakiongozwa na kaulimbiu inayosema ‘‘Usawa Wa Kijinsia Katika Umiliki Wa Ardhi Kwa Ustawi Wa Jamii Yetu’’
Akifungua mkutano huo Machi 6, 2024 mkoani Tabora, Dkt. Batilda Burian amesema wadau hao wamepata muda mwafaka wa kujadili mwelekeo wa jinsi mradi utakavyotekelezwa na kujadiliana namna bora ya kutatua changamoto zitakazojitokeza klatika halmashauri zao.
“Mkutano huu umekuja muda muafaka katika mkoa wetu hasa mwezi huu wa Machi ambao unaenda sanjari na Siku ya Wanawake Duniani yanayoongozwa na kaulimbiu inayosema ‘‘Wekeza kwa Wanawake Kuharakisha Maendeleo ya Taifa na Ustawi wa Jamii’’ ni ni heshima kubwa mradi huu kutekeleza katika Wilaya zetu” amesema Balozi Dkt. Batilda.
Mradi huo unatekelezwa katika mkoa wa Tabora katika halmashauri za Kaliua, Sikonge, Uyui, Urambo, Nzega Mjini, Nzega Vijijini na Manispaa ya Tabora.
Mkuu wa Mkoa amesisitizitiza kuwa Mkoa huo upo mstari wa mbele katika kutekeleza mradi wa Uboreshaji wa Usalama wa Milki za Ardhi kwa maendeleo ya wananchin wa Mkoa huo.
Aidha, Mkuu wa Mkoa amewataka wataalamu wa sekta ya ardhi washirikiane na viongozi wa Serikali za mitaa na vijiji kuwapa wananchi elimu kuhusu masuala ya ardhi ili kutoa taarifa sahihi ambazo zitasaidia kurahisisha utekelezaji wa mradi huo.
Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa LTIP Bw. Joseph Shewiyo amesema mradi huo unalenga kupanga matumizi ya ardhi kwa maendeleo ya vijiji na miji, kuhamasisha umiliki wa ardhi kwa pamoja, kuzingatia haki za makundi maalum katika umiliki wa ardhi pamoja na usawa wa kijinsia katika umiliki wa ardhi.
Bw. Shewiyo ameongeza kuwa hadi sasamradi huo umeongeza idadi ya wanawake wanaomiliki ardhi kutoka asilimia 25 hadi 38 hali inayosaidia kufikia azma ya Serikali ya kuwaletea wananchi usawa wa kijinsia katika umiliki wa ardhi.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa