Waziri wa Madini, Mhe. Anthony Mavunde, amezindua kiwanda cha kuzalisha nishati mbadala ya mkaa (briquettes) kiitwacho Rafiki Briquettes, kilichopo Kata ya Kiloleni, Manispaa ya Tabora, hatua inayolenga kuongeza ajira na kulinda mazingira.
Kiwanda hicho, kilichojengwa na Shirika la Madini la Taifa, Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), kina uwezo wa kuzalisha tani 20 za mkaa mbadala kwa saa moja kwa kutumia mchanganyiko wa vumbi la makaa ya mawe, teknolojia inayotarajiwa kupunguza matumizi ya nishati isiyo rafiki kwa mazingira.
Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mkuu wa Wilaya ya Tabora, Mhe. Upendo Wella, amesema uwekezaji huo ni utekelezaji wa maelekezo ya Rais na sehemu ya mkakati wa Serikali kukuza uchumi wa viwanda mkoani humo.
“Kiwanda hiki kitakuwa mkombozi katika suala la ajira. Takribani ajira 200 zinatarajiwa kupatikana hapa. Huu ni ushindi kwa Mkoa wa Tabora kwa kuwa maelekezo ya Mhe. Rais yametekelezwa kwa vitendo,” alisema Mhe. Wella.
Kwa mujibu wa Waziri Mavunde, uzalishaji wa mkaa mbadala utasaidia kupunguza shinikizo la ukataji miti, kuboresha usafi wa mazingira na kurahisisha upatikanaji wa nishati kwa matumizi ya majumbani na viwandani.
Uzinduzi huo umeshuhudiwa na Mwenyekiti wa Bodi ya STAMICO nchini, Mhe. Simon Sirro, pamoja na viongozi wa Serikali ngazi ya mkoa na wilaya pamoja na wadau wa sekta ya madini na mazingira.
Hatua hiyo inaifanya Tabora kuwa miongoni mwa mikoa inayoongoza katika utekelezaji wa miradi ya nishati mbadala inayochochea maendeleo ya viwanda huku ikihifadhi mazingira kwa vizazi vijavyo.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa