Na. Mwandishi Wetu – Tabora.
Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, Dkt. John Mboya, amefungua kikao kazi cha tathmini ya utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini (TASAF Awamu ya Tatu – TASAF III), kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mtemi Isike Mwanakiyungi, katika ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora.
Katika hotuba yake ya ufunguzi, Dkt. Mboya aliwapongeza wataalamu wa TASAF kutoka halmashauri zote za mkoa kwa juhudi na weledi waliouonesha katika utekelezaji wa awamu ya tatu ya mpango huo, akieleza kuwa kazi yao imechangia kwa kiasi kikubwa kufikia malengo ya mpango wa kupunguza umaskini kwa walengwa.
"Mnatekeleza mpango huu kwa bidii na weledi wa hali ya juu. Mmewezesha kufikiwa kwa malengo yaliyowekwa, niwaombe muendelee na moyo huo wa kuwahudumia Wananchi hususan Kaya Maskini," alisisitiza Dkt. Mboya.
Aidha, alifafanua namna Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inavyoendelea kuthibitisha dhamira yake ya dhati kwa wananchi kwa kupeleka fedha za kutosha kutekeleza shughuli mbalimbali za TASAF. Tangu kuanzishwa kwa mpango huo mwaka 2015, mafanikio makubwa yameripotiwa, hususan katika kipindi cha Julai 2024 hadi Mei 2025, ambapo jumla ya kaya 41,604 katika vijiji 721 na mitaa 153 mkoani Tabora zimenufaika na mpango huo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa katika kikao hicho, zaidi ya Shilingi bilioni 8.08 zimehawilishwa moja kwa moja kwa walengwa katika kipindi hicho, fedha ambazo zimeleta tija na mabadiliko chanya katika maisha ya wananchi wa Tabora.
Katika mawasilisho kutoka kwa waratibu wa TASAF wa halmashauri mbalimbali, imebainika kuwa utekelezaji wa mpango huo umeleta mafanikio makubwa katika maeneo mengi ya mkoa kwa kuimarisha maisha ya watu, kuongeza fursa za ajira na kuinua shughuli za kiuchumi za kijamii.
Miongoni mwa maazimio ya kikao hicho ni pamoja na kuimarisha zaidi mikakati ya kuwafikia walengwa kwa ufanisi mkubwa ili kuendelea kupunguza umasikini kwa kasi zaidi. Washiriki wa kikao walisisitiza umuhimu wa kuendeleza usimamizi madhubuti na uwazi katika matumizi ya rasilimali zinazotolewa na serikali na wadau wa maendeleo.
Mwisho.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa