Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Richard Abwao, amefungua rasmi mashindano ya Umoja wa Michezo wa Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA) kwa mwaka 2025 katika viwanja vya Shule ya Wavulana Tabora, akihimiza nidhamu, uzalendo, na mshikamano miongoni mwa wanamichezo hao.
Akisoma risala ya ufunguzi kwa niaba ya Kamati ya maandalizi ya michezo hiyo, Afisa Elimu Michezo Mkoa wa Tabora, Mwl. Hassan Katuli, alieleza kuwa zaidi ya michezo saba itashindaniwa katika mashindano hayo, ikiwemo mpira wa miguu, pete, wavu, kikapu, mikono, riadha pamoja na sanaa za maonesho.
Mashindano haya yanahusisha Halmashauri zote nane za Mkoa wa Tabora, yakiwa yamevutia jumla ya washiriki 960 — wasichana 509 na wavulana 451. Aidha, wanamichezo hao wameandamana na timu ya walimu wa michezo, walezi, na madaktari wapatao 144 (wanaume 111 na wanawake 33).
Akitoa salamu za Mkoa, Katibu Tawala Msaidizi anayeshughulikia Elimu, Bi. Upendo Rweyemamu, alisisitiza kuwa lengo kuu la mashindano haya ni kubaini vipaji bora vitakavyoiwakilisha Tabora katika mashindano ya kitaifa yatakayofanyika mkoani Iringa kuanzia tarehe 18 hadi 30 Juni, 2025. Aliongeza kuwa nidhamu ni msingi mkuu wa mashindano haya na hatua kali zitachukuliwa dhidi ya yeyote atakayekiuka taratibu.
Akihutubia hadhira, Kamanda Abwao alitoa shukrani kwa wadau wote waliowezesha kufanikisha mashindano hayo, akitambua mchango wao wa hali na mali. Alieleza kuwa michezo imeendelea kuwa kichocheo muhimu cha fursa, ikiwemo ajira, kuimarisha afya ya mwili na akili, kukuza moyo wa uzalendo na kuleta mshikamano wa kitaifa.
Hata hivyo, alibainisha changamoto kadhaa zinazokwamisha ustawi wa michezo shuleni, zikiwemo uhaba wa vifaa, bajeti ndogo, na mwamko hafifu kutoka kwa wazazi na walezi. Alitoa rai kwa wadau mbalimbali wa michezo, wazazi, na watendaji wa elimu kutambua umuhimu wa michezo na sanaa katika maendeleo ya kijamii na kitaaluma.
“Naomba wadau wote wa michezo Mkoa wa Tabora kuendelea kuchangia maendeleo ya michezo yetu. Wazazi, waone umuhimu wa michezo kwa watoto wenu na wawaruhusu kushiriki kikamilifu. Watendaji katika shule zetu hakikisheni masomo ya michezo na sanaa yanapewa kipaumbele,” alisema Kamanda Abwao.
Aidha, aliwahimiza wanamichezo kuonesha juhudi na nidhamu ya hali ya juu, huku akitoa wito kwa waamuzi kutenda haki ili kusaidia kupatikana kwa timu bora ya Mkoa wa Tabora. Alimalizia kwa kuwahakikishia usalama wa kutosha kwa washiriki wote wakati wa mashindano hayo.
Mashindano haya yanasimamiwa kwa pamoja na Wizara ya TAMISEMI, Elimu pamoja na Utamaduni, Sanaa na Michezo, yakibeba kauli mbiu ya mwaka huu:
“Viongozi Bora ni Msingi wa Maendeleo ya Taaluma, Sanaa na Michezo — Shiriki Uchaguzi Mkuu 2025 kwa Amani na Utulivu.”
Mwisho.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa