MKUU wa Mkoa wa Tabora Dkt. Philemon Sengati amewaongoza wanakijiji cha Igombe kilichopo Manispaa ya Tabora kupanda miti zaidi ya 300 ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha miaka 59 ya uhuru wa Tanzania bara.
Zoezi hilo limefanyika katika eneo la Mistu ya Hifadhi ya Bwawa la Igombe ambacho ni miongoni mwa vyanzo vya maji ya Bwawa la Igombe ambalo litaoa huduma ya maji katika Manispaa ya Tabora.
Mkuu wa Mkoa wa Tabora Dkt. Sengati aliendesha zoezi hilo ikiwa ni sehemu ya kuadhimisha miaka 59 ya uhuru wa Tanzania bara kwa kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii.
Akizungumza baada ya kupanda miti kwenye eneo hilo la Hifadhi ambalo liloathiriwa na shughuli za kibinadamu ikiwemo kilimo , uchomaji mkaa na ufugaji aliwataka viongozi wa Wilaya zote kuhakikisha wanafikisha lengo la Kitaifa la kupanda miti milioni 1.5 kila mwaka.
Alisema Ofisi yake itahakikisha inafuatilia ili kupata takwimu sahihi na ikibainika kuwa ipo Wilaya ambayo hakufikia lengo la Kitaifa , hatasita kuwachukulia hatua viongozi.
Aidha Mkuu huyo wa Mkoa aliwataka Wakala wa Mistu Tanzania kwa kushirikiana na Mamalaka ya maji safi na Usafi wa Mazingira Tabora , Manispaa ya Tabora , Bonde la Tanganyika na wananchi katika kulinda na kuhakikisha usalama wa Hifadhi ya Mistu ya Igombe kwa ajili ya kuwahakikisha wakazi wa Manispaa ya Tabora uendelevu wa upatikanaji wa maji kutoka Chanzo cha Bwawa la Igombe.
Aliwataka wadau mbalimbali wanaosimamia uhifadhi wa Msitu huo kuendelea kutoa elimu kwa wakazi wanaozunguka maeneo ya Hifadhi ya Msitu huo kuendelea kuulinda na kuwaondoa wavamizi kwa kuzingatia misingi ya Sheria na taratibu.
Katika hatua nyingine Dkt. Sengati alisema wakati wa zoezi la upandaji wa miti ni vema wakapanda miti ya miembe na mikorosho ili pamoja na kulinda mazingira waweze kupata kipato kutokana na uuzaji wa maembe na korosho.
Alisema mpango wa Mkoa ni kuanzisha mashamba makubwa ya miembe na mikorosha katika eneo la Tura wilayani uyui kwa ajili ya kuwavutia wawekezaji wa viwanda vya kushindika matunda kuchukua na kuanzisha viwanda mkoani humo.
Kaimu Katibu Tawala Msaidizi Uchumi na Uzalishaji Abrahaman Mdeme alisema katika msimu wa mwaka 2019/20 , Mkoa wa Tabora ulipanda miti laki 7.3 na iliyopona ni laki 4.5 .
Alitaja sababu zilizopelekea miti mingi kutopona ni pamoja na kushambuliwa na mifugo, kuchomwa moto , ukame na baadhi ya wananchi kupanda miti kipindi cha mwisho wa msimu wa mvua.
Mhifadhi wa Mistu wa Mnaispaa ya Tabora Peter Kisanga alisema Msitu wa Hifadhi wa Bwawa la Igombe una ukubwa wa Hekta 7,501 ni chanzo maji katika Bwawa la Igombe ambalo ndio linatoa huduma kwa wakazi wa Manispaa ya Tabora.
Alisema kuna baadhi ya watu wamekuwa wakivamia Msitu huo wa hifadhi kwa ajili ya shughuli mbalimbali ya kujitafutia kipato kinyume na Sheria zinazoulinda.
Kisanga aliuomba Uongozi wa Mkoa na Kamati ya Usalama ya Mkoa wa Tabora kushirikiana nao katika kuwaondoa watu ambao wamekuwa wakihatarisha uendelevu wa msitu huo na Bwawa la Igombe kwa kuendelea kilimo katika maeneo ambayo hayatakiwi, uvuvi haramu na ukataji wa magogo na uchomaji wa mkaa.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa