Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mhe. Paulo Matiko Chacha, ameongoza na kufungua rasmi kongamano la wafanyabiashara wadogo mkoani humo lililofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Utumishi wa Umma – Uhazili, ambapo amewataka wananchi wa Tabora kuchangamkia kwa ujasiri fursa za kiuchumi zinazotolewa na Serikali kupitia mfumo wa manunuzi ya umma (NeST) pamoja na kuchangamkia mitaji kupitia mikopo isiyo na riba inayotolewa na serikali.
Akitoa neno la utangulizi, Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, Dkt. John Mboya, alimshukuru Mhe. Chacha kwa kukubali kuwa mgeni rasmi, akisisitiza kuwa kongamano hilo lina umuhimu mkubwa kwa ustawi wa kiuchumi wa wananchi, hususan wafanyabiashara wadogo. “Jukwaa hili ni mahsusi kwa ajili ya kuwawezesha ninyi wananchi kutambua fursa nyingi ambazo serikali yetu imeziweka kupitia sera na sheria mbalimbali, hivyo ni muhimu kusikiliza kwa makini ili tuweze kunufaika nazo,” alisisitiza Dkt. Mboya.
Akitoa salamu kutoka Mamlaka ya Udhibiti na Ununuzi wa Umma (PPRA) makao makuu, Meneja wa PPRA Kanda ya Magharibi na Kati, Mhandisi Suma Atupele, alieleza kuwa kifungu cha 64 cha Sheria ya Ununuzi wa Umma na Kanuni ya 35 kinatoa mwongozo wa namna zabuni za serikali zinavyopaswa kutekelezwa kwa makundi maalum, yakiwemo wanawake, vijana, wazee na watu wenye ulemavu. Alibainisha kuwa ni wajibu wa kila taasisi za serikali kutenga angalau asilimia 30 ya zabuni kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo, hivyo akatoa wito kwa wananchi kujisajili ili kunufaika na fursa hiyo adhimu.
Mratibu wa Mfuko wa Programu za Uwezeshaji kutoka NEEC, Ndg. Samwel Shikona, alisema serikali imeweka miongozo na sheria thabiti za kuwawezesha wananchi kiuchumi. Alibainisha jukumu lao kubwa ni kuwaunganisha wananchi na fursa zilizopo nchi nzima ili washiriki kikamilifu katika maendeleo ya taifa.
Akihutubia washiriki wa kongamano hilo, Mhe. Chacha aliwasisitiza wananchi kujenga kujiamini na kuchukua hatua madhubuti katika kuchangamkia fursa hizo. “Kwanza tujiamini na kuwa serious. Wataalamu wapo kutusaidia, tuhakikishe tunajisajili ili hizo fursa za asilimia 30 zisitupite. Hali ya usalama wa mkoa wa Tabora ipo shwari, tuchangamkie fursa, tufanye biashara na kujipatia kipato. Hakuna hela ya muujiza; wewe fanya kazi. Mganga wa kienyeji hawezi kukuletea pesa, hebu fanyeni yale ambayo serikali inawaambieni,” alisisitiza Mhe. Chacha.
Kongamano hilo limejikita katika kuhamasisha wananchi, hasa wafanyabiashara wadogo wa Tabora, kushiriki kikamilifu kwenye fursa za kiuchumi na kimaendeleo zinazotolewa na serikali kupitia sera na mifumo rasmi ya manunuzi na uwezeshaji.
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa