SERIKALI KUKARABATI MAENEO YA HARAKATI ZA UKUMBOZI ILI KULINDA HISTORIA
SERIKALI imesema inatafuta fedha kwa ajili ya kukarabati maeneo yote yaliyopo Tanzania ambayo yaliyotumika katika harakati za kudai uhuru na ukombozi katika nchi mbalimbali barani Afrika ili kutunza historia yake isipotee.
Kauli hiyo imetolewa jana Wilayani Kaliua na Waziri wa Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Dkt Harrison Mwakyembe wakati wa ziara yake ya kutembelea maeneo ya urithi wa ukombozi wa bara la Afrika ikiwemo eneo la Shujaa wa Afrika Mashariki na Kati Mtemi Mirambo.
Waziri alisema kuwa lengo ni kutaka historia ya mashujaa na maeneo waliyotumia isipotee ili kuwafanya vijana wa sasa na vizazi vijavyo viwe na ukweli wa historia za mashujaa wote.
Alisema ukarabati huo unakwenda sanjari na kutafuta kumbukumbu zote walizotumia wapiganiauhuru mbalimbali kwa ajili kuzitambua na kuzihifadhi rasmi kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo ili kulinda historia isije ikapotea.
Dkt. Mwakyembe alitoa wito kwa watanzania wote wenye taarifa za kumbukumbu mbalimbali zikiwemo picha, vitabu, mashairi, nyimbo, barua na nyaraka mbalimbali zilizotumiwa na wapiganiauhuru wa Tanzania na nje ya Nchi kuwasilisha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo au kwa viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa ili ziweze kutunzwa kwa ajili ya manufaa ya Nchi na bara la Afrika kwa ujumla.
Aidha aliwataka wananchi na Viongozi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha wanalinda alama zote zilizopo katika maeneo yaliyotumiwa na wapigania uhuru ikiwemo majina katika makaburi na majengo ili kutopoteza kumbukumbu za mashujaa.
Katika hatua nyingine, Waziri huyo aliwataka wataalamu mbalimbali wakiwemo Maafisa Utamaduni kuhakikisha wanatumia hazina ya wazee waliopo ambao wanajua historia ya kweli kuhusu harakati za kudai uhuru nchini na mapambano ya ukombozi barani Afrika kupata maelezo na kuyaandika kwa ajili ya kuweka kumbukumbu ili zisitoweke.
“Tunajua kila mtu atakufa hivyo ni vema tukatumia hazina ya wazee wetu waliopo sasa kupata historia ya kudai uhuru na harakati za ukumbozi zilizofanyika nchini ili kuweka kumbukumbu zote” alisema.
Alisema simulizi ya wazee ni muhimu katika kuhakikisha hakuna mashujaa walioshiriki harakati za kudai uhuru na ukombozi wa bara la Afrika watakaoachwa katika kumbukumbu za historia.
Mwisho
Tabora
S.L.P: 25 Tabora
Simu: 026 2604058
Mobile:
Barua Pepe: ras.tabora@tamisemi.go.tz
Haki Miliki ©2017 Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Tabora .Haki zote zimehifadhiwa